Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MAISHA YA FURAHA!



“MBEGU ZA UZIMA”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Februari 1, 2026 
Juma la 4 la Mwaka A wa Kanisa

Sef 2: 3; 3: 12-13; 
Zab 146: 6-10; 
1Kor 1: 26-31; 
Mt 5: 1-12.


MAISHA YA FURAHA!

Sisi wote tunapenda kuwa na furaha, na huwa tunajishughulisha kwa hatima hii katika hali mbali mbali. Masomo ya leo yanatuonesha jinsi ya kuwa na maisha ya furaha. Lakini ni kinyume na jinsi tunavyo fikiria. Huwa tunajua kuwa maskini, kuwa mpole na kuonewa haviongozi kwenda kwenye maisha ya furaha. Ila kujiinua kwa ukuu wetu, mafanikio yetu, maisha yanayo zalisha, majivuno yanaongoza kwenye maisha ya furaha.

Katika somo la kwanza tunasikia kuishi katika maisha ya umaskini wa roho maana yake kuishi kwa unyenyekevu itatuongoza kwenda kwenye furaha. Na katika somo la pili tunasikia Mt. Paulo akitujulisha kwamba uchaguzi wa Mungu ni tofauti na uchaguzi wa Mwanadamu wanaofanya. Mungu anachagua wale wanyonge katika jamii na dhaifu mbele ya uso wa Ulimwengu ili kuwanyenyekesha wenye majivuno. Leo katika injili tunamuona Yesu akihutubia mlimani, akitupa njia za kuwa na furaha. Yesu kwa kupitia “heri” anatupa njia sahihi za kuingia kwenye furaha. Zinatuongoza kwanza, katika uhusiano na Mungu na hapo ni Mungu atakaye tubariki ili tuwe na maisha ya furaha. Zinaonesha wazi kwamba sio mwanadamu anaye ongoza kwenye furaha bali ni Mungu na hali zetu kumwelekea yeye. 

Katika masomo ya Noeli, Yesu alifunuliwa kama Mwana wa Kifalme wa Daudi na Mwana wa Mungu. Kama Musa alivyowaongoza Waisraeli kupitia bahari ya Shamu na kuwapa sheria ya Mungu katika mlima Sinai, Yesu pia amepita katika maji ya ubatizo na sasa katika Injili, anaenda Mlimani kutangaza sheria mpya- sheria ya ufalme wake. Heri hizi zina ashiria ukamilifu wa Agano la Mungu alilo mwahidia Abrahamu- kwamba kupitia uzao wake mataifa yote yatapokea Baraka za Mungu (Mwa 12:3; 22:18).

Heri hizi sinatufunulia njia ya Kimungu na malengo ya maisha yetu. Kujitahidi kwetu kote kunapaswa kuwa kwa fadhila hizi-kwa maskini wa roho; wanyenyekevu na wenye moyo safi; wenye huruma na watengenezaji wa Amani, watafuta haki inayotoka katika sheria ya Ufalme wa Mungu. Njia ambayo Mungu ameiweka mbele yetu leo ni njia yenye majaribu na mateso. Lakini ana ahidi kutufariji katika huzuni na kutupa thawabu kubwa. 

Heri hizi zipo katika mtiririko wa pekee, kuanzia heri ya kwanza ambayo heri maskini wa roho. Ni kwa kuanza kwa kuwa mnyenyekevu mbele ya Mungu na kuruhusu upendo wa Mungu uingie katika maisha yetu. Kwani kwa unyenyekezu wa roho utatufanya tuvumilie yote, kuonewa na kuteswa na kujitahidi katika maisha yetu. Na mwisho wa yote tutapata raha na kuridhika. Mungu amechagua kuwabariki wanyonge na wadogo, wale wanao onekana wajinga na wasiopendwa katika macho ya dunia, kama anavyosema Paulo katika somo la pili. Wale maskini wa roho ni wale wanao fahamu kwamba hawawezi kufanya chochote na kufanikiwa pasipo huruma na neema ya Mungu. 

Sisi tupo katika kipindi ambacho tunavutwa sana na raha na kujiridhisha kwa starehe za dunia, kuwa na mali nyingi na mafanikio makubwa. Haya yote yanatupa hali ya shauku kubwa. Lakini ukweli ni kwamba hatujawahi kuridhika na kila kukicha tunatafuta zaidi na zaidi. Tajiri mkubwa, bado anahitaji zaidi, ana kila kitu katika maisha lakini bado hana raha ya maisha. Tumeona maisha ya matajiri wengi katika dunia, hawajawahi kuridhika, daima wanatafuta ili aweze kuwa juu ya wengine na kwa hili hana raha anahangaika daima. 

Jumapili iliopita masomo yaliongelea kuhusu wito wetu wa pamoja wa kuwa wafuasi. Tumepewa wito wa kuwa mwanga kwa ulimwengu. Na leo Yesu, anatupa mwanga-maneno ya uzima wa milele. Yesu anatuonesha sisi njia ambayo tunaweza kuiishi sio maneno matupu pekee. Kwasababu yeye mwenyewe aliishi heri zote tangu kuzaliwa mpaka ufufuko wake. Ni njia ya kuelekea kwenye maisha ya furaha ambayo ni maisha ya uzima wa milele. Sio safari rahisi, kwani twaweza kukumbana na umaskini katika maisha, kuumizwa, kuteseka kwa sababu ya haki na kuuonewa. Lakini, ni pale ambapo tutafungua mioyo yetu kwa Yesu tunaweza kupata furaha na kuridhika katika maisha ambayo anatupa sisi kutoka katika upendo wake usio na mwisho. 

Heri ni kipimo kamili cha maisha ya furaha na zaidi sana maisha yetu ya Kikristo. Zinatuita kwenda sehemu yenye faraja kamili. Tunapaswa kuwa jasiri na kuwa tayari kwenda kinyume na yale mambo ya wakati huu yanayo pingana na “heri”, tuwe tayari kusema “hapana” kwa maisha ya raha za muda tu na kutupilia mbali tamaduni mbaya, ambazo kwa ukweli zinatupa raha ya muda tu katika maisha. 

Sala: Bwana, ninaomba niweze kukumbatia “heri” zote ulizo tupatia sisi. Ninasali, zaidi sana , moyo wangu uweze kukua katika unyenyekevu. Ninaomba ukue katika kuwaonea huruma wanao onewa, wanao umizwa, waliochanganyikiwa na waliobanwa na maisha ya dhambi. Ninakushukuru kwa Baraka unazoendelea kunipa. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 1, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 1, 2026
DOMINIKA YA 4 YA MWAKA A


MWANZO:
Zab. 106:47

Ee Bwana Mungu wetu, utuokoe, utukusanye kwa kututoa katika mataifa, tulishukuru jina lako takatifu, tuzifanyie shangwe sifa zako.


SOMO 1
Sef. 2:3, 3:12 – 13

Mtafuteni Bwana, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya Bwana.

Lakini nitasaza ndani yako watu walioonewa na masikini, nao watalitumainia jina la Bwana. Mabaki ya Israeli hawatatenda uovu, wala kusema uongo; wala ulimi wa hadaa hautaonekana kinywani mwao; kwa maana watakula na kulala, wala hapana mtu atakayewaogofya.

Neno la Mungu… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 146:6b – 10 (K) Mt. 5:3

(K) Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao.

Huishika kweli milele.
Huwafanyia hukumu walioonewa,
Huwapa wenye njaa chakula;
Bwana hufungua waliofungwa. (K)

Bwana huwafumbua macho waliopofuka;
Bwana huwainua walioinama;
Bwana huwapenda wenye haki;
Bwana huwahifadhi wageni. (K)

Huwategemeza yatima na mjane;
Bali njia ya wasio haki huipotosha.
Bwana atamiliki milele,
Mungu wako, Ee Sayuni, kizazi hata kizazi. (K)



SOMO 2
1Kor. 1:26 – 31

Ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu. Bali kwa yeye ninyi mmepata kuwa katika Kristo Yesu, aliyefanywa kwetu hekima itokayo kwa Mungu, na haki, na utakatifu, na ukombozi; kusudi, kama ilivyoandikwa, Yeye aonaye fahari na aone fahari juu ya Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Yn. 14:5

Aleluya, aleluya,
Tomaso akamwambia Bwana, Sisi hatujui uendako, nasi twaijuaje njia?
Aleluya.



INJILI
Mt. 5:1-12

Yesu alipowaona makutano, alipanda mlimani; na alipokwisha kuketi, wanafunzi wake walimjia; akafumbua kinywa chake, akawafundisha, akisema,
Heri walio maskini war oho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao.
Heri wenye huzuni; maana hao watafarijika.
Heri wenye upole; maana hao watairithi nchi.
Heri wenye njaa na kiu ya haki;
Maana hao watashibishwa.
Heri wenye rehema; maana hao watapata rehema.
Heri wenye moyo safi; maana hao watamwona Mungu.
Heri wapatanishi; maana hao wataitwa wana wa Mungu.
Heri wenye kuudhiwa kwa ajili ya haki; maana ufalme wa mbinguni ni wao.
Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMWAMINI YESU KWA MAISHA YETU!



ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, Januari 31, 2026
JUMA LA 3 LA MWAKA 

2 Sam 12:1-7.10-17;
Zab 51:10-15
Mk 4: 35-41

KUMBUKUMBU YA MT. YOHANE BOSCO


KUMWAMINI YESU KWA MAISHA YETU!


Bahari na mawimba yana mtii Mungu kwasababu ni sehemu ya uumbaji wake. Na wala hakuna tatizo kubwa sana kwa Mungu ambalo anashindwa kulitatua. Hofu zetu hazina mwisho, matatizo yetu yanatusumbua, kwasababu sisi wenyewe tumechagua kuyakabili wenyewe kwa nguvu zetu. Wafuasi walikuwa ni watu wa kawaida kama sisi. Hata wakiwa kati ya Yesu wana ogopeshwa na gharika! Laiti kama Mwanadamu angelijua kukabidhi hofu zake na maumivu yake kwa Mungu! 

Ni rahisi sana kukata tamaa katika maisha. Ni rahisi zaidi kuelekeza mwelekeo wote kwenye matatizo na kuacha mengine yanayo tuzunguka. Hata kama ingekuwa ni maneno ya hasira na ya kuumiza kutoka kwa wengine, matatizo ya kifamilia, matatizo ya umma, ukosefu wa fedha nk. Kuna kila sababu ya kila mmoja wetu kuanguka kwenye mtego wa hofu, kuchanganyikiwa, kuumia na kuwa na shauku. Lakini ilikuwa ni kwasababu ya sababu hizi Yesu aliruhusu tukio hili litokee akiwa na wafuasi wake. Alikuwa kwenye boti na wafuasi wake akaruhusu wafuasi wakumbwe na gharika kuu, wakati yeye akiwa amelala, ili aweze kuleta ujumbe wa kufaa kwetu sisi wote. 

Katika habari hii, wafuasi walilenga kwenye kitu kimoja tuu: walikuwa waangamie! Bahari ilikuwa ikiwasukasuka na waliogopa maangamizi makubwa! Lakini kwa kupitia yote hayo, Yesu alikuwa pale akionekana amelala, akiwasubiri waweze kumwamsha. Na walipo mwamsha, alikemea gharika na hali ikawa shwari. Hili ni kweli pia katika maisha yetu. Sisi mara nyingi tunaruhusu matatizo mengi tunayopata yatutese na kutusukasuka. Ufunguo ni kwamba tunapaswa kugeuza macho yetu na kumwelekea Yesu. Muone mbele yako amelala, anakusubiri umwamshe. Yupo daima, akikusubiri na yupo tayari daima. Kumwamsha Bwana wetu ni rahisi kama ilivyo rahisi kugeuza macho yetu kutoka katika gharika na kusadiki uwezo wake wa Kimungu. Yote ni kuwa na Imani kwake tu. Imani kamili. Je, una mwamini yeye? Tumwache Yesu achukue nafasi ya kila kitu katika maisha yetu tuliopo. Anatupenda na kweli atatujali wote. 

Sala: Bwana, ninakugeukia katikati ya changamoto za maisha na ninatamani kukuamsha uje katika maisha na kunisaidia. Ninatambua upo daima karibu yangu, ukinisubiri mimi nikuamini wewe kwa kila kitu. Nisaidie nielekeze macho yangu kwako na kuwa na Imani kamili katika mapendo yako. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JANUARI 31, 2026







MASOMO YA MISA, JANUARI 31, 2026
JUMAMOSI YA JUMA LA 3 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MT. YOHANE BOSCO


SOMO 1
2 Sam. 12:1-7, 10-17

Bwana alimtuma Nathani aende kwa Daudi. Naye akamwendea, akamwambia, Palikuwa na watu wawili katika mji mmoja; mmoja wao alikuwa tajiri, wa pili maskini. Yule tajiri alikuwa na kondoo na ng’ombe wengi sana; bali yule maskini hakuwa na kitu, ila mwana-kondoo mmoja, mdogo, ambaye amemnunua na kumlea; naye akakua pamoja naye, na pamoja na wanawe; hula sehemu ya posho lake, na kukinywea kikombe chake, na kulala kifuani mwake, akawa kwake kama binti. Hata msafiri mmoja akamfikilia yule tajiri, naye akaacha kutwaa mmoja wa kondoo zake mwenyewe au mmoja wa ng’ombe zake mwenyewe, ili kumwandalia yule msafiri aliyemfilia, bali alimnyang’anya yule maskini mwana-kondoo wake, akamwandalia yule mtu aliyemfikilia. 

Ndipo hasira ya Daudi ikawaka sana juu ya mtu yule; akamwambia Nathani, Aishivyo Bwana, mtu huyo aliyetenda jambo hili, hakika yake astahili kufa; naye atamrudishia yule mwana-kondoo mara nne, kwa sababu ametenda neno hili, na kwa sababu hakuwa na huruma. 
Basi, Nathani akamwambia Daudi, Wewe ndiwe mtu huyo. Basi, sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau, ukamtwaa mkewe Uria, Mhiti, kuwa mke wako.

Bwana asema hivi, Angalia, nitakuondokeshea uovu katika nyumba yako, anmi nitawatwaa wake zako mbele ya macho yako, na kumpa jirani yako, naye atalala na wake zako mbele ya jua hili. Maana wewe ulifanya jambo lile kwa siri; bali mimi nitalifanya jambo hili mbele ya Israeli wote na mbele ya jua.

Daudi akamwambia Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi. Nathani akamwambia Daudi, Bwana naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa. Lakini, kwa kuwa kwa tendo hili umewapa adui za Bwana nafasi kubwa ya kukufuru, mtoto atakayezaliwa kwako hakika yake atakufa. Naye Nathani akatoka kwenda nyumbani kwake.

Basi Bwana akampiga yule mtoto ambaye mkewe Uria alimzalia Daudi, naye akawa hawezi sana. Basi Daudi akamwomba Mungu kwa ajili ya mtoto; Daudi akafunga, akaingia, akalala usiku kucha chini. Nao wazee wa nyumba yake wakondoka, wakasimama karibu naye, ili wamwinue katika nchi; lakini hakukubali, wala hakula chakula pamoja nao.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:10-15 (K) 12

(K) Ee Mungu, uniumbie moyo safi.

Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako takatifu usiniondolee. (K)

Unirudishie ya wokovu wako,
Unitegemeze kwa roho ya wepesi.
Nitawafundisha wakosaji njia zako,
Na wenye dhambi watarejea kwako. (K)

Ee Mungu, Mungu wa wokovu wangu,
Uniponye na damu za watu,
Na ulimi wangu utaiimba haki yako.
Ee Bwana, uifumbue midomo yangu,
Na kinywa changu kitazinena sifa zako. (K)


SHANGILIO
Yn. 3:16

Aleluya, aleluya,
Jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee, ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele.
Aleluya.


INJILI
Mk. 4:35-41

Siku ile kulipokuwa jioni, Yesu akawambia, Na tuvuke mpaka ng’ambo. Wakauacha mkutano, wakamchukua vile vile alivyo katika chombo. Na vyombo vingine vilikuwako pamoja naye. Ikatokea dhoruba kuu ya upepo, mawimbi yakakipiga chombo hata kikaanza kujaa maji. Naye mwenyewe alikuwapo katika shetri, amelala juu ya mto; wakamwamsha, wakamwambia, Mwalimu, si kitu kwako kuwa tunaangamia? Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu. Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga? Hamna Imani bado? Wakaingiwa na hofu kuu, wakaambiana, Ni nani huyu, basi, hata upepo na bahari humtii?

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUSIMIKA UFALME WA MUNGU!

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, 30 Januari 2026,
Juma la 3 la mwaka

2 Sam 11: 1-10, 13-17;
Zab. 51: 3-7, 10-11;
Mk 4: 26-34.

KUSIMIKA UFALME WA MUNGU!

Leo tena Yesu anaongelea jambo jingine, mtu aliepanda mbegu ardhini nakuisubiri ichipue nakumea mpaka ichanue nakuwatayari kwa mavuno. Hajui ni jinsi gani inavyoota lakini anavuna wakati wa mavuno utimiapo.

Yesu pia anaongelea kuhusu punje ya Haradali ambayo ni ndogo sana lakini hukuwa na kuwa mmea mkubwa, hata kuwa na msitu wakuweza kukaa ndege juu yake na kuweka viota ndani yake.

Mfano huu unaelezea maadili au ukweli wa kiroho ambao Yesu alikuwa akiwafundisha wafuasi, kwamba yeye anafanya nini na wao inawapasa wafanye nini wakati utakapo timia. Neno hili ambalo ni ujumbe na nafsi ya Yesu lina nguvu, linatawala kwa nguvu sehemu nyingi na linapenya na kuwa kitulizo kinacho wajenga wengine na kuwalinda na kuwahifadhi wadogo katika dunia yetu.

Ufalme wa Mungu unafanya kazi namna hiyo hiyo kati yetu, bila hata kutambua kwa akili zetu, lakini je, tupo tayari kuvuna katika shamba hili la neema au tupo tayari kulala katika shamba la dhambi lililo jaa majani? Je tunatambua kuwa tunaweza kutenda jambo jema dogo sana likakua likaleta neema kwako na kwa wengine?

Sala :Bwana, naomba nioteshe matendo mema, ili yaweze kuwa mavuno ya Neema kwa watu wote. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JANUARI 30, 2026

 

MASOMO YA MISA, JANUARI 30, 2026

IJUMAA YA 3 MWAKA


SOMO 1

2 Sam. 11:1-10, 13-17


Ikawa, mwanzo wa mwaka mpya, wakati watokapo wafalme kwenda vitani, Daudi akampeleka Yoabu, na watumishi wake pamoja naye, na Israeli wote; wakawaangamiza wana wa Amoni, wakauhusuru Raba. Lakini Daudi mwenyewe akakaa Yerusalemu.

Ikawa wakati wa jioni, Daudi akaondoka kitandani, akatembea juu ya dari ya jumba la mfalme; na alipokuwa juu ya dari aliona mwanamke anaoga; naye huyo mwanamke alikuwa mzuri sana, wa kupendeza macho. Naye Daudi akapeleka, akauliza habari za yule mwanamke. Mtu mmoja akasema, Je! Huyu siye Bath-sheba, binti Eliamu, mkewe Uria, Mhiti? Basi Daudi akapeleka wajumbe, akamtwaa; naye akaingia kwake; naye akalala naye; (maana yule mwanamke amekwisha kutakasika unajisi wake); kasha akarudi nyumbani kwake. Yule mwanamke akachukua mimba; basi akapeleka na kumwambia Daudi, akasema, Ni mjamzito.

Ndipo Daudi akapeleka kwa Yoabu, akisema, Unipelekee Uria, Mhiti. Naye Yoabu akampeleka Uria kwa Daudi. Uria alipomwendea DAudi, Daudi alimwuliza habari za Yoabu, na habari za watu, na habari za vita. Daudi akamwambia Uria, Hay, shuka nyumbani mwako, ukanawe miguu yako. Basi Uria akatoka katika nyumba ya mfalme, na tunu ya vyakula ikamfuata, iliyotoka kwa mfalme. Lakini Uria akalala mlangoni pa nyumba ya mfalme, pamoja na watumishi wote wa bwana wake, wala hakushuka nyumbani kwake.

Watu walipomwambia Daudi ya kwamba, Uria hakushuka nyumbani kwake. Naye Daudi akamwalika, akala, akanywa mbele yake; naye akamlevya; hata wakati wa jioni akatoka kwenda kulala kitandani mwake pamoja na watumishi wa bwana wake, lakini hakushuka nyumbani kwake.

Hata ikawa asubuhi, Daudi akamwandikia Yoabu waraka, akaupeleka kwa mkono wa Uria. Akaandika katika waraka huo, kusema, Mwekeni Uria mbele ya watu penye vita vikali, kasha ondokeni, mmwache, ili apigwe, akafe. Ikawa Yoabu alipokuwa akiuhusuru mji, akamweka Uria mahali alipojua ya kuwa pana mashujaa. Watu wa mji wakatoka, wakapigana na Yoabu; na baadhi ya watu, watumishi wa Daudi, wakaanguka; Uria Mhiti naye akafa.


Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI

Zab. 51: 1-5, 8-9 (K) 1


(K) Uturehemu, Ee Mungu, kwani tumekosa.


Ee Mungu, unirehemu, sawasawa na fadhili zako;

Kiasi cha wingi wa rehema zako,

Uyafute makosa yangu.

Unioshe kabisa na uovu wangu,

Unitakase dhambi zangu. (K)


Maana nimejua mimi makosa yangu,

Na dhambi yangu I mbele yangu daima.

Nimekutenda dhambi Wewe peke yako,

Na kufanya maovu mbele za macho yako.

Wewe ujulikane kuwa una haki unenapo

Na kuwa safi utoapo hukumu.

Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu,

Mama yangu alinichukua mimba hatiyani. (K)


Unifanye kusikia furaha na shangwe,

Mifupa uliyoipondwa ifurahi.

Usitiri uso wako usitazame dhambi zangu,

Uzifute hatiya zangu zote. (K)


SHANGILIO

Mt. 11:25


Aleluya, aleluya,

Utukuzwe, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa umewafunulia watoto wachanga mafumbo ya ufalme wa mbingu.

Aleluya.


INJILI

Mk. 4:26-34


Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ufalme wa Mungu, mfano wake ni kama mtu aliyemwaga mbegu juu ya nchi; akawa akilala na kuondoka, usiku na mchana, nayo mbegu ikamea na kukua, asivyojua yeye. Maana nchi huzaa yenyewe; kwanza jani, tena suke, kisha ngano pevu katika suke. Hata matunda yakiiva, mara aupeleka mundu, kwa kuwa mavuno yamefika.

Akasema, Tuulinganishe na nini ufalme wa Mungu? Au tuutie katika mfano gani? Ni kama punje ya haradali, ambayo ipandwapo katika nchi, ingawa ni ndogo kuliko mbegu zote zilizo katika nchi, lakini ikiisha kupandwa hukua, ikawa kubwa kuliko miti yote ya mboga, ikafanya matawi makubwa; hata ndege wa angani waweza kukaa chini ya uvuli wake.

Kwa mifano mingi ya namna hii alikuwa akisema nao neno lake, kwa kadiri walivyoweza kulisikia; wala pasipo mfano hakusema nao; lakini akawaeleza wanafunzi wake mwenyewe mambo yote kwa faragha.


Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MWANGA WENU UANGAZE

 


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Januari 29, 2026
JUMA LA 3 LA MWAKA
Ebr 10: 19-25;
Zab 24: 1-6;
Mk 4: 21-25
------------------------------------------------
MWANGA WENU UANGAZE

Leo Yesu anatualika kuwa mwanga. Mwanga unaondoa giza mbele yetu. Anatualika pia tusimame mahali ambapo nasi tutaonekana kama taa. Naamini huu wito wakuwa mwanga una nyanja mbili.
Kwanza kabisa katika hali ya mtu binafsi. Kila mmoja wetu amepokea mwanga, ambao ni Roho wa Mungu aliye ndani mwetu. Mwanga unapoingia sehemu yeyote unaonekana. Vivyo hivyo hata maisha ya kiroho. Tunatambua kujielewa wenyewe zaidi. Kila kilichofichwa hutoka kwenye mwanga kama Yesu anavyosema katika mstari wa 22. Hili pia linabeba pia muonekana wa dhambi zetu. Ni kazi ya Roho wa Mungu kuvumbua dhambi na kuturudisha (ref. Yn 16:8-11). Tunachopata kuona ni kile kilichokuwa ndani yetu muda wote, ambacho kilikuwa hakionekana kwasababu hakukuwa na mwanga wa kutosha. Sasa Roho Mtakatifu anatuwezesha sisi tuweze kutambua kile kisicho chema na chenye maadili mabaya na kutuonesha matokeo yake mbaya. Kwa kusaidiwa na mwanga wa Roho Mtakatifu tunaanza kukuwa na kuelewa kile tulichoitiwa.
Sehemu ya pili ni maisha ya pamoja. Taa inapowekwa kwenye kinara haijiangazii peke yake. Bali nikwa ajili ya wengine. Badala ya kujikita katika kujiweka wema peke yetu tujitahidi pia kuwasaidia wengine. Hili ndilo somo la kwanza linalosisitiza. Tunapaswa kufahamu ni kwa jinsi gani tunapaswa kusaidiana kwa mapendo ili kujenga kazi njema. Hatupaswi kujitenga na wengine kama wengine wanavyofanya, bali tupeane moyo (Ebr 10:24). Umoja wetu ni kwa jili ya nini? Tunawezaje kusaidiana kwa mapendo na kuleta kazi njema?

Tafakari leo, juu ya maisha ya ukarimu. Kuna njia nyingi mno jinsi ya kuwa mkarimu kwa mwenzako. Jikite katika maisha ya wema na tenda yale yote anayotaka Mungu ndani mwako.
Sala: Bwana, nisaidie mimi niweze kuwa mkarimu katika mapendo yangu na mwenye huruma juu ya wengine. Roho wa Mungu angaza ndani mwangu, ili niweze kujitambua mimi ni nani, nisaidie mimi niweze kuwasaidia wengine wajitambue ya kwamba wao ni nani katika kweli. Yesu nakuamini wewe. Amina
Copyright ©2013-2026©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JANUARI 29, 2026


 


MASOMO YA MISA, JANUARI 29, 2026 ALHAMISI, JUMA LA 3 LA MWAKA SOMO 1 2 Sam. 7:18-19, 24-29 Daudi, mfalme, aliingia, akaketi mbele za Bwana, akasema, Mimi ni nani, Bwana Mungu, na nyumba yangu ni nini, hata umenileta hata hapa? Tena jambo hili lilikuwa dogo machoni pako, Ee Bwana Mungu; hata umeleta habari ya nyumba yangu mimi, mtumwa wako, kwa miaka mingi inayokuja baadaye; na hayo kwa namna ya kibinadamu, Ee Bwana Mungu. Nawe ulijifanyia imara watu wako Israeli, wawe watu wako milele; nawe, Bwana, umekuwa Mungu wao.
Basi sasa, Ee Bwana Mungu, neno lile ulilolinena katika habari za mtumwa wako, na katika habari za nyumba yangu, ulifanye imara milele, ukatende kama ulivyosema. Jina lako na litukuzwe milele, kusema, Bwana wa majeshi ndiye Mungu juu ya Israeli; na nyumba ya mtumwa wako, Daudi, itakuwa imara mbele zako. Kwa kuwa wewe, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, umenifunulia mimi, mtumwa wako, ukisema, Nitakujengea nyumba; kwa hiyo mimi, mtumwa wako, nimeona vema moyoni mwangu nikuombe dua hii. Na sasa, Ee Bwana Mungu, wewe ndiwe Mungu, na maneno yako ndiyo kweli, nawe umemwahidia mtumwa wako jambo hili jema; basi, sasa, uwe radhi, ukaibarikie nyumba ya mtumwa wako, ipate kudumu milele mbele zako; kwa maana wewe, Ee Bwana Mungu, umelinena; na kwa Baraka yako nyumba ya mtumwa wako na ibarikiwe milele. Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI Zab. 132:1-5, 11-14 (K) Lk. 1:32 (K) Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, Baba yake. Bwana, umkumbukie Daudi Na taabu zake zote alizotaabika. Ndiye aliyemwapia Bwana, Akaweka nadhiri kwa shujaa wa Yakobo. (K) Sitaingia hemani mwa nyumba yangu, wala sitapanda matandiko ya kitanda changu; sitaacha macho yangu kuwa na usingizi wala kope zangu kusinzia, hata nitakapompatia Bwana mahali, na shujaa wa Yakobo maskani (K) Bwana amemwapia Daudi neno la kweli, hatarudi nyuma akalihalifu, baadhi ya wazao wa wmili wako nitawaweka katika kiti chako cha enzi. (K) Wanao wakiyashika maagano yangu, na shuhuda nitakazowafundisha, watoto wao nao wataketi katika kiti chako cha enzi milele. (K) Kwa kuwa Bwana ameichagua Sayuni, ameitamani akae ndani yake. Hapo ndipo mahali pangu pa raha milele, Hapo nitakaa kwa maana nimepatamani. (K)
SHANGILIO Zab. 119:105 Aleluya, aleluya, Neno lako ni taa ya miguu yangu, ee Bwana, na mwanga wa njia yangu. Aleluya. INJILI Mk. 4:21-25 Yesu aliwaambia wafuasi wake: Mwaonaje? Taa huja ili kuwekwa chini ya pishi, au mvunguni? Si kuwekwa juu ya kiango? Kwa maana hakuna neno lililositirika, ila makusudi lije likadhihirika; wala hakuna lililofichwa, ila makusudi lije likatokea wazi. Mtu akiwa na masikio ya kusikia, na asikie. Akawaambia, Angalieni msikialo; kipimo kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa, na tena mtazidishiwa. Kwa maana mwenye kitu atapewa, naye asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang’anywa. Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MBEGU NI NENO LA MUNGU




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
JANUARI 28, 2026

JUMA LA 3 LA MWAKA WA KANISA

Kumbukumbu ya Mt. Tomas Aquinas

2 Sam 2:4-17
Zab 89:3-4.26-29,
Mk 4:1-20

MBEGU NI NENO LA MUNGU

“lakini waliopanda katika udongo mzuri ni wale waliosikia neno la Mungu na kulikubali na kuliacha lizae matunda”. 

Katika Injili ya Marko ambayo ni fupi kati ya Injili nne, huwa inatazama kazi za Yesu zaidi kuliko mahubiri yake, tunapaswa kuchukulia kwa makini mafundisho ambayo anayachukua Marko katika Injili yake. Tunaweza kuchukulia mifano aliochagua Marko kama iliyo ya muhimu kabisa. 

Injili ya leo ina sehemu tatu muhimu. Sehemu ya kwanza naya mwisho inaelezea Yesu akitoa mfano na kuuelezea. Katikati Yesu anaelezea kwanini yeye anahubiri kwa mifano. Karibia sura nne za injili ya Marko zimebeba mifano, na Injili ya leo ya Marko imebeba mistari 20 ya sura ya nne. Hivyo mfano wa leo ni wa muhimu kweli kweli. 

Mpanzi ni Mungu Baba. Anayesia neno lake kwa kila mtu, hata kule kuko onekana kuwa kama ujinga kwasababu ya kusia mbegu zake hata katika mioyo migumu ya watu, hiki ni kipimo cha upendo wake kwa kila mtu. Anawapatia watu wake neno hata wale walio na mioyo migumu kama mwamba au jiwe, hata wale waliosongwa na ulimwengu, hata wale ambao machoni mwa mwanadamu hawafai. Changamoto hapa ni kwamba tunapaswa kulima na kutifua udongo wa mioyo yetu ili neno la Mungu liote na kuweka mizizi. Na pia tunapaswa kulipalilia linapo anza kukuwa kwa kufweka miiba (malimwengu yanayo tusonga), ili neno liweze kuzaa matunda mema na kuwafikia wote. 

Neno hili likizaa matunda watu watachuma matunda ya neema na kumshukuru Mungu kwa ajili ya zawadi ya mazao ya neno lake. Mmoja akilipokea neno la Mungu akampenda Mungu na jirani, hata jirani watampa Mungu shukrani kwasababu ya neno lililo ingia ndani ya nafsi ya huyo mtu kiasi cha kuzaa matunda yakawafikia wengine. 

Sala: Ee Mungu ninakuomba Neno la Mwanao lizame ndani ya moyo wangu lizae matunda ya upendo, Amani, furaha na utulivu wa kuungana nawe na pia niweze kuwaleta wengine kwako kutokana na matunda yake. Yesu nakutumaini .Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JANUARI 28, 2026



MASOMO YA MISA, JANUARI 28, 2026
JUMATANO, JUMA LA 3 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MT. TOMAS AQUINUS


SOMO 1
2 Sam. 7:4:17

Neno la Bwana lilimfikia Nathani kusema, Enenda, ukamwambie mtumishi wangu, Daudi, Bwana asema hivi, Je! Wewe utanijengea nyumba, nikae ndani yake? Kwa maana mimi sikukaa ndani ya nyumba, tangu siku ile niliyowatoa wana wa Israeli katika Misri, hata leo, lakini nimekaa katika hema na maskani. Mahali mwote nilimokwenda na wana wa Israeli wote, je! Nimesema neno lolote na mtu yeyote wa waamuzi wa Israeli, niliyemwagiza kuwalisha watu wangu Israeli, niliyemwagiza kuwalisha watu wangu Israeli, nikisema, Mbona hamkunijengea nyumba ya mierezi?

Basi, sasa, mwambie mtumishi wangu, Daudi, maneno haya, Bwana wa majeshi asema hivi, Nalikutwaa katika zizi la kondoo, katika kuwaandama kondoo, ili uwe mkuu juu ya watu wangu, juu ya Israeli; nami nimekuwa pamoja nawe kila ulikokwenda, na kuwakatilia mbali adui zako wote mbele yako; nami nitakufanyia jina kuu, kama jina la wakuu walioko duniani. Tena nitawaagizia mahali watu wangu Israeli, nami nitawapanda, wapate kukaa mahali pao wenyewe, wasiondolewe tena; wala wana wa uovu hawatawatesa tena, kama hapo kwanza; naam, kama vilivyokuwa tangu siku ile nilipowaamuru waamuzi, wawe juu ya watu wangu Israeli; nami nitakustarehesha mbele ya adui zako wote.

Tena Bwana anakuambia ya kwamba Bwana atakujengea nyumba. Nawe siku zako zitakapotimia, ukalala na baba zako, nitainua mzao wako nyuma yako, atakayetoka viunoni mwako, nami nitaufanya imara ufalme wake. Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele. Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu, akitenda maovu nitamwadhibu kwa fimbo ya binadamu na kwa mapigo ya wanadamu; lakini fadhili zangu hazitamwondoa mbele yako. Na nyumba yako, na ufalme wako, vitathibitishwa milele mbele yako. Nacho kiti chako kitafanywa imara milele.

Kwa maneno hayo yote, na kwa maono hayo yote, na kwa maono hayo yote, ndivyo Nathani alivyonena na Daudi.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 89:3-4, 26-29 (K) 28

(K) Hata milele nitamwekea fadhili zangu.

Nimefanya agano na mteule wangu, 
Nimemwapia Daudi mtumishi wangu.
Wazao wako nitawafanya imara milele,
Nitakijenga kiti chako cha enzi hata milele. (K)

Yeye ataniita: Wewe Baba yangu,
Mungu wangu na mwamba wa wokovu wangu.
Nami nitamjalia kuwa mzaliwa wangu wa kwanza,
Kuwa juu sana kuliko wafalme wa dunia. (K)

Hata milele nitamwekea fadhili zangu,
Na agano langu litafanyika amini kwake.
Wazao wake nao nitawadumisha milele.
Na kiti chake cha enzi kama siku za mbingu. (K)


SHANGILIO

Aleluya, aleluya,
Mbegu ni neno la Mungu, anayepanda ni Kristo; atakayemkuta, ataishi milele.
Aleluya.


INJILI
Mk. 4:1-20

Yesu alianza kufundisha tena kando ya bahari. Wakamkusanyikia mkutano mkubwa mno, hata yeye akapanda chomboni, akakaa baharini; mkutano wote ulikuwako juu ya nchi kavu kando ya bahari. Akawafundisha mambo mengi kwa mifano, akawaambia katika mafundisho yake, Sikilizeni; Tazama, mpanzi alitoka kwenda kupanda; ikawa alipokuwa akipanda, mbegu nyingine ilianguka kando ya njia, wakaja ndege wakaila. Nyingine ikaanguka penye mwamba, pasipokuwa na udongo mwingi; mara ikaota kwa kuwa na udongo haba; hata jua lilipozuka iliungua, na kwa kuwa haina mizizi ikanyauka. Nyingine ikaanguka penye miiba; ile miiba ikamea, ikaisonga, isizae matunda. Nyingine zikaanguka penye udongo ulio mzuri, zikazaa matunda, zikimea na kukua, na kuzaa, moja thelathini, moja sitini, na moja mia. Akasema, Aliye na masikio ya kusikia, na asikie.

Naye alipokuwa peke yake, wale watu waliomzunguka, na wale Thenashara, walimwuliza habari za ile mifano. Akawaambia, Ninyi mmejaliwa kuijua siri ya ufalme wa Mungu, bali kwa wale walio nje yote hufanywa kwa mifano, Ili wakitazama watazame, wasione, na wakisikia wasikie, wasielewe; wasije wakaongoka, na kusamehewa.
Akawaambia, Hamjui mfano huu? Basi mifano yote mtaitambuaje? Mpanzi huyo hulipanda neno. Hawa ndio walio kando ya njia, lipandwapo neno; nao, wakiisha kusikia, mara huja Shetani, akaliondoa lile neno lililopandwa mioyoni mwao. Kadhalika na hawa ndio wapandwao penye miamba, ambao kwamba wakiisha kulisikia lile neno, mara hulipokea kwa furaha; ila hawana mizizi ndani yao, bali hudumu muda mchache; kisha ikitokea dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara hujikwaa. Na hawa ndio wale wapandwao penye miiba, ni watu walisikiao lile neno, na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali, na tamaa za mambo mengine zikiingia, hulisonga lile neno, likawa halizai. Na hawa ndio waliopandwa penye udongo ulio mzuri; ni watu walisikialo lile neno na kulipokea, na kuzaa matunda, mmoja thelathini, mmoja sitini, na mmoja mia.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.